*Tukio la kutekwa Ludovick ladaiwa kuwa ni 'feki'
*RB yake yazua utata, Polisi washikwa kigugumizi
JIMEIBUKA hofu ya kuwepo mpango mahususi unaoratibiwa na Serikali
kufichua njama za kigaidi, ambazo zinadaiwa kutekelezwa na baadhi ya
viongozi wa kisiasa wanaoheshimika katika jamii, MTANZANIA Jumapili
limebaini.Taarifa za uhakika zilizolifikia gazeti hili zinaeleza kuwa,
kukamatwa kwa mtuhumiwa namba mbili katika kesi ya ugaidi iliyofunguliwa
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Ludovick Joseph, ni utekelezaji wa
mpango huo.
Imedaiwa kuwa, kuna utata mkubwa wa usahihi wa taarifa za tukio la
Ludovick kutekwa na watu ambao hawajafahamika hadi sasa na hata taarifa
za kutekwa kwake alizodai kuzifikisha katika kituo kidogo cha polisi
Kigogo, nazo zina utata.
Kwa mujibu wa wapasha habari wetu, taarifa za kutekwa kwa Ludovick na
kunyang’anywa vitu vyake vyote alivyokuwa navyo, zikiwemo nguo alizokuwa
amevaa na hata madai kuwa aliripoti tukio hilo katika kituo cha Polisi
Kigogo siyo za kweli, bali zimetengenezwa ili kufanikisha mpango huo.
Ludovick alidai kutekwa usiku wa Jumanne ya Machi 5, mwaka huu, akiwa
eneo la Sinza ambako alisema alitoa taarifa zake katika Kituo cha Polisi
cha Kigogo na kufunguliwa RB yenye namba KIG/RB/318/2013.
Taarifa ya kutekwa kwake aliiandika mtandaoni na ilisomeka hivi; ‘Leo
usiku, yapata saa tano na nusu, niliachana na Maggid Mjengwa maeneo ya
Shekilango tukitokea Rose Garden. Yeye alielekea hotelini alikofikia
sehemu fulani Kariakoo nami nikasubiri kigari kuelekea nyumbani kwangu.
Hapo Shekilango, magari yalichelewa kidogo, pembeni ilipaki bajaji ikiwa
na watu wawili na dereva ndipo wakaniambia twende tuchangie mia tano tu
kwenda Ubungo Mataa, nikakaa katikati ya hao jamaa.
Ghafla wakakata kona na kuanza kuelekea Mabibo huku wakiulizana kama
wako kamili na mwingine kujibu yuko kamili. Nikajua tayari niko mikononi
mwa majambazi na sikujua wako kamili namna gani, kwa hiyo nikaamua kuwa
mtulivu.
Tulipofika relini karibu na Mabibo wakanipokonya begi lakini,
hawakulifungua. Ndani yake kulikuwa na laptop, toshiba kubwa na chaji
yake, kamera ndogo ya digital na USB yake, modem ya zantel na card
reader. Tulipofika maeneo ya Loyola Sekondari, nikawasihi wanishushe ili
nirudi mwenyewe, wakaniambia safari ile inaishia Jangwani.
Nikaingiwa na wasiwasi mkubwa na nia yao hasa, maana wameshanipokonya
begi kwa nini wasiniachie? Lakini niliendelea kuwa mtulivu ili
kutowaprovoke.
Tulipovuka Kigogo mwisho kwenye giza karibu na msikiti, wakasimama
pembeni ya barabara na kuniamuru kushuka, nikashuka na kuanza kuwadai
begi langu, ndipo mmoja akasema wamekuwa wastaarabu mimi naanza
kuwadharau. Ghafla akanivuta kwa nguvu kunirudisha kwenye kibajaji
akamwambia mwenzie wanisachi kama nina vitu vingine, wakanisachi na
kuchukua pesa, nilikuwa na elfu 35 na simu mbili ndogo za nokia moja
yenye line mbili.
Kisha mmoja akatoa ‘order’ nivuliwe nguo. Nikavuliwa viatu, T-shirt na
suruali nikabaki na nguo za ndani pekee. Wakanishusha na kuniacha hapo.
Kurudi nyuma kama hatua kumi tu ndipo kituo kidogo cha polisi Kigogo
nikaanza kutoa maelezo hapo kwa zaidi kama ya saa mbili nikiwa uchi na
nguo za ndani tu. Nikiwa hapo nikasikia polisi wakiwasiliana juu ya
tukio la kupigwa vibaya Absalom Kibanda, kwenye redio calls.
Ilikuwa yapata saa nane, baada ya kuchukuliwa maelezo polisi walinipatia
gari nikaelekea hotelini kwa Maggid, ambaye saa kumi aliamshwa na
kunichukulia chumba hapo nikapumzika. Ameniazima nguo zake ndizo nimevaa
bado hadi sasa naelekea kituo cha Polisi Magomeni kwenda kupewa
mpelelezi wa kesi yangu. Namba ya kesi yangu Kigogo ni KIG/RB/318/2013,
wizi kutoka maungoni.’
Wakati Ludovick akiwa ametoa maelezo hayo kwa jamii kupitia mitandao ya
kijamii, polisi wameshindwa kuthibitisha taarifa za kutekwa, kuporwa na
kupokea taarifa yake aliyodai kuitoa kituo kidogo cha polisi Kigogo.
Polisi katika kituo kidogo cha Kigogo waliohojiwa na MTANZANIA Jumapili
kuhusiana na taarifa za Ludovick, walionekana kurushiana mpira
kuzizungumzia.
Askari aliyekutwa kituoni hapo alipoulizwa kuhusu taarifa hizo alisema
taarifa za matukio mbalimbali hufunguliwa hapo, lakini huhamishiwa Kituo
cha Polisi cha Magomeni kutokana na udogo wa kituo hicho, hivyo kumtaka
Mwandishi kufuatilia suala hilo katika Kituo cha Polisi Magomeni.
Gazeti hili lilipofika Kituo cha Polisi Magomeni, kwa Askari Mpelelezi
liliyeelekezwa kuwa anahusika na kesi ya Ludovick aliyetajwa kwa jina
moja la Chuki hakuwepo bali lilipewa namba ya simu yake ya kiganjani na
alipotafutwa, naye alikana kuhusika na suala hilo na kuelekeza atafutwe
askari polisi aliyetajwa kwa jina la Lukwamba Sanga.
Alipopigiwa Sanga na kuulizwa kuhusu sakata hilo, kwanza alikiri kuwa
yeye ndiye mpelelezi wa kesi hiyo na kueleza kuwa ni kweli Ludovick
alifungua RB katika kituo cha Polisi cha Kigogo lakini hakuwa tayari
kutoa namba ya RB hiyo.
Alieleza kuwa mwenye mamlaka ya kutoa namba hiyo ni Mkuu wa Upelelezi wa
Kituo ambaye hata hivyo hakupatikana, lakini ofisa mwingine kituoni
hapo alieleza kuwa namba hiyo inaweza kutolewa kwa idhini ya Kamanda wa
Mkoa wa Polisi Kinondoni, Charles Kenyela.
Kamanda Kenyela alipotafutwa, alisema anahitaji muda kuipata namba hiyo,
kwa sababu ana majukumu mengi hivyo atafutwe baadaye. Lakini
alipotafutwa tena simu yake ya kiganjani ilikuwa haipatikani.
Hata alipopigiwa simu tena jana iliita mfululizo pasipo majibu.
Wachambuzi wa masuala ya saikolojia wanadai dalili zinaonyesha kuwapo
kwa uwezekano wa Ludovick kushiriki tukio la kutekwa na kupigwa kwa
Mhariri Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, ambaye pia ni
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, Absalom Kibanda.
Wanasema ni kawaida kuwa watu wanaojihusha na matukio ya aina hii, baada
ya kuyatekeleza huchanganyikiwa, hivyo hata kitendo cha Ludovick
kukimbilia kuandika katika mtandao wa ‘facebook’ kuwa naye alitekwa
kinaweza kuchukuliwa katika mtizamo huo.
Maswali ya kujiuliza
Ikiwa ni zaidi ya mwezi mmoja sasa baada ya kuvamiwa na kuteswa kwa
Kibanda na siku chache baadaye kukamatwa kwa Ludovick akihusishwa na
tuhuma za kupanga ugaidi, yapo maswali mengi miongoni mwa jamii ambayo
hayajapata majibu kuhusu matukio hayo.
Swali kubwa linaloumiza vichwa vya wengi hivi sasa ni namna ambavyo
Ludovick alifanikiwa kujipenyeza na kufanikiwa kujenga mtandao wa
masiliano ya simu za mkononi na katika mitandao ya kijamii na Wahariri
mbalimbali wa Vyombo vya Habari.
Tayari Wahariri wawili, Deodatus Balile na Ansbert Ngurumo,
wamekwishatajwa kuwa na mawasiliano ya muda mrefu na Ludovick na kwamba
kuna baadhi ya taarifa muhimu za waandishi na wahariri ambazo Ludovick
alikuwa akizipata kupitia mawasilino yake hayo.
Kutajwa kwa wahariri hao kuwa washirika wa karibu kimawasiliano na
Ludovick, kuliibua hisia kuwa Wahariri hao, waliingizwa katika mtandao
wa Ludovick na kuanza kufanya kazi zake pasipo wao wenyewe kujua au
wakiwa na ufahamu huo.
Lakini pia wadadisi wa mambo wamekuwa wakihoji nguo za Ludovick zilipo
baada ya kile kinachodaiwa kuwa tukio hilo la kudai kutekwa ni feki.
Hali kadhalika hatua ya Ludovick baada ya kuachana na Mjegwa na kupanda
bajaji iliyokuwa na watu wawili kisha akakaa katikati kwa nauli ya
shilingi mia tano huku akiwa na pesa taslimu shilingi 35,000, begi lenye
laptop toshiba kubwa, chaja yake, kamera ndogo ya digital na USB yake,
modem ya zantel na card reader, jambo linaloonyesha kuwa alikuwa na
uwezo wa kuchukua usafiri salama zaidi.
Aidha, mkanganyiko wa maelezo ya Ludovick na yale yaliyotolewa na
Mjengwa ambako yeye (Ludovick) alidai kupewa gari na polisi kumpeleka
hotelini kwa Maggid, huku Maggid akidai alifika hapo kwa usafiri wa
teksi, nayo yanazidi kuacha swali gumu la kupata ukweli wa sakata hili
zima.
Kuhusishwa kwake na tukio la Kibanda Siku na wakati ambao Kibanda
alitekwa na kuteswa, Ludovick naye alidai kutekwa na majambazi akiwa
eneo la Sinza, jirani na mahali ilipo ofisi ya Kibanda. Ludovick alidai
kutekwa na watu wasiojulikana majira ya saa tano usiku siku ya Jumanne
ya Machi 5, mwaka huu, ambapo watekaji wake walimnyang’anya vitu vyake
mbalimbali na kumvua nguo zote pamoja na kuchukua simu zake mbili.
Ingawa katika uchunguzi wake gazeti hili liliambiwa kuwa simu yake
iliendelea kutumika katika maeneo ya mnara wa Sinza karibu na ofisi
anakofanyia kazi Kibanda siku mbili mara baada tukio la kuteswa kwa
Mhariri huyo. Pamoja na hilo, siku mbili kabla Kibanda hajatekwa,
anadaiwa kufanya mawasiliano na kiongozi mmoja mkubwa wa chama cha
siasa.
Ahusishwa na video ya Lwakatare
Yuko mikononi mwa sheria na alishafikishwa Mahakamani pamoja na
Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema), Wilfred Lwakatare, kutokana na mipango ya kudhuru watu,
wakiwemo waandishi wa habari pamoja na suala la ugaidi.
Inaelezwa kuwa watu hao wamekuwa karibu kwa muda mrefu ambapo wote ni
wenyeji wa Mkoa wa Kagera, na kwa mujibu wa watu wa karibu na mahusiano
yao, walisema kuwa Ludovick amepata kumsaidia kufanya kampeni za kuwania
ubunge wa Jimbo la Bukoba Mjini mwaka 2000.
Ludovick ni nani?
Ludovick, mbali na kuwa na ukaribu na Lwakatare, pia alikuwa mtu wa
karibu na Mjengwa, akimsaidia katika shughuli za blog yake, pamoja na
wahariri mbalimbali wa habari.
Ludovick pia wapo wanaomtambua kama mtu wa Idara ya Usalama wa Taifa.
Mjengwa pia aliwahi kukiri kutofahamu kazi halisi aliyokuwa akiifanya
Ludovick mtaani, lakini katika maelezo yake aliyoandika kupitia kwenye
mtandao wa Jamii Forum, Mjengwa alisema anamfahamu Ludovick tangu akiwa
Chuo Kikuu (DUCE) na kwamba ni mmoja wa Watanzania wengi waliomfahamu
kupitia kazi zake magazetini.