Saturday, April 20, 2013

‘Viroba’ tishio jipya saratani ya koo kwa wanaume

 

Daktari bingwa wa uchunguzi wa magonjwa ya saratani katika Kitengo cha Patholojia, Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk Henry Mwakyoma na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Dk Crispin Kahesa wameeleza hayo jijini Dar es Salaam.
Walisema kuwa ingawa bado hakuna visababishi kamili vya saratani hiyo, asilimia 90 ya wagonjwa wa saratani ya koo wamekuwa na historia ya uvutaji sigara, unywaji pombe kali kama viroba na kula aina za vyakula vilivyochomwa ikiwamo nyama na samaki, ulaji pilipili, ndimu, ‘chilisosi’ na unywaji wa vitu vya moto kupita kiasi.
“Ongezeko ni kubwa, asilimia 90 ya wagonjwa tuliowapokea hapa wana historia ya kutumia vilevi vikali, sigara, pilipili kwa wingi na aina nyingine na vitu vinavyosababisha saratani hii,” anasema Dk Kahesa.
Anasema kuwa Saratani ya Koo ni mbaya zaidi ukilinganisha na saratani za aina nyingine.
Anaeleza: “Saratani ya Koo ni mbaya ukimwona mgonjwa unaweza kulia, hawezi tena kula na ikibidi huingiziwa mipira maalumu ili kupitisha chakula, lakini kuna wakati hata mipira huziba, hivyo huishi kwa dripu ya chakula pekee.”
Naye Dk Mwakyoma anaeleza kuwa Saratani ya Koo hushambulia seli zinazotanda koo na kutengeneza uvimbe katikati ya koo ambao huanza kuleta madhara taratibu.
“Ukiwa na Saratani ya Koo, itakuchukua muda mrefu sana mpaka kuanza kuona viashiria mbalimbali, awali mgonjwa huanza kupata shida kumeza chakula. Wengi hufika hapa wakiwa wamechelewa na tunavyofanya vipimo huwa katika hatua mbaya sana,” anasema Mwakyoma.
Anazitaja aina kuu mbili za Saratani ya Koo kuwa ni: “Oesophagus Carcinoma na Squamous cell carcinoma, ambazo hutofautiana kulingana na jinsi seli zake zinavyoonekana kwenye darubini.
Hata hivyo, pamoja na tofauti hizo za mwonekano, utambuzi na matibabu ya aina hizi za Saratani ya Koo hufanana.”
Anabainisha kuwa aina zote mbili huanza kwa kuathiri seli zilizo katika utando wa ndani wa ukuta wa koo, uitwao ‘mucosa’ kabla ya kusambaa maeneo mengine.
Kwa upande wake Dk Kahesa anasema kuwa katika hatua za awali, mgonjwa mwenye Saratani ya Koo anaweza asionyeshe dalili zozote. Hata hivyo, kadiri saratani inavyozidi kukua na kuenea, mgonjwa anaweza kuanza kuona dalili.
“Dalili ya kwanza ya mgonjwa wa saratani ni chakula kukwama kwenye koo, siku za mwanzo mgonjwa anaweza kushindwa kumeza chakula kigumu kisha cha majimaji na baadaye akashindwa kumeza hata mate.



Love to hear what you think!