Tuesday, June 2, 2015

Dk Slaa: "Watanzania Wanataka Safari ya Uhakika na Siyo ya Matumaini......Chagueni UKAWA Maana ni Safari ya Uhakika"


Katibu Mkuu wa Chadema, Dk  Willibrod Slaa amesema Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), mwaka huu, unaingia kwenye uchaguzi ukiwa na safari ya uhakika na siyo ya matumaini kama ilivyotolewa na mmoja wa watangaza nia ya kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu ujao. 
 
Dk Slaa alisema, kauli hiyo ni moja kati ya nyingi zinazotolewa na viongozi wengi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambazo Watanzania wamechoka kuzisikia na badala yake wanahitaji vitendo.
 
Alitoa kauli hiyo juzi mjini Tunduma wilayani Momba mkoani Mbeya, alipokuwa akihutubia wakazi wa mji huyo katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Shule ya Msingi Tunduma.
 
Dk Slaa alisema Watanzania wanahitaji safari yenye uhakika wa maendeleo ambayo watayapata Oktoba, mwaka huu, kupitia upinzani lakini siyo  kutoka kwa kiongozi yeyote wa CCM.
 
“Eti safari ya matumaini, hivi kweli Tanzania iliyojaa kila aina ya madini na utajiri wa kutisha halafu tunasema safari ya matumaini badala ya vitendo? Watanzania tumechoka na kauli za matumaini, tumechoka kuishi kwa matumaini katika nchi yetu,” alisema Dk Slaa.
 
Mbali na hilo, Dk Slaa  aliwashangaa baadhi ya watangaza nia wa CCM walioiponda Serikali yao kwamba imeshindwa wakati wao ndio walitakiwa kuwa mstari wa mbele kuondoa kero hizo.
 
Ukawa wajipanga
Akizungumza kuhusu Ukawa walivyojipanga kuingia Ikulu Oktoba mwaka huu, Dk Slaa alisema wana akiba ya kutosha ya viongozi makini wa kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi.
 
Alisema wakishika dola hawatakuwa na sababu yoyote ya kukopa viongozi kutoka kwa CCM.
 
“Hatuna njaa ya viongozi ndani ya upinzani, tunao wa kutosha. Hatuna haja ya kwenda CCM kuwakopa viongozi, Oktoba tupeni ridhaa upinzani tubadili sura ya nchi,” alisema. 
 
Kwa upande wake Mbunge wa Mbozi Magharibi (Chadema), David Silinde alisema, licha ya Serikali ya CCM kuamua kugawa majimbo katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kujiokoa, hawataambulia kitu kwani wamejipanga kukabiliana na hali yoyote itakayojitokeza.
 
“CCM tumewagundua na janja yao, baada ya kuona wabunge wao wamekabwa koo, ndio wanatafuta njia mbadala ya kujiokoa kwa kugawa majimbo, lakini tunasema majimbo yote yaliyopendekezwa kugawanywa Mbeya kama yatapitishwa tunachukua yote,” alisema Silinde.



Love to hear what you think!