Tuesday, February 19, 2013

MAUAJI YA PADRI ZANZIBAR NYUMA YA PAZIA

Na Haruni Sanchawa
MAUAJI ya Padri wa Kanisa Katoliki Zanzibar, Evarist Mushi yaliyotokea juzi (Jumapili) wakati akiingia kanisani kuendesha ibada ya asubuhi, yamezua utata na inadaiwa kuna mambo mengi yaliyojificha nyuma ya pazia.
Akina mama wakilia kwa uchungu kuomboleza kifo cha ghafla cha kupigwa risasi Padri Evarist Mushi kilichotokea juzi asubuhi.
Mauaji hayo yalifanyika kimafia katika Kanisa Katoliki, Kigangwe cha Mtoni saa 12:45 asubuhi wakati akijiandaa kwenda kuongoza ibada kanisani humo.
Kwa mujibu wa ofisa mmoja wa polisi, katika eneo la tukio walifanikiwa kukuta maganda mawili ya risasi na hakukuwa na wizi wowote uliofanyika baada ya padri huyo kupigwa risasi mbili kichwani.
Waumini wa Kanisa Katoliki Zanzibar na wananchi wa mjini Zanzibar wakikusanyika kwenye hospitali kuu ya Mnazimmoja mjini Zanzibar wakitafakari kuhusu tukio la Padri Evarist Mushi kuuawa kwa kupigwa rirasi juzi mjini Zanzibar.
Mashuhuda waliozungumza na Mwandishi kwa nyakati tofauti walisema sababu zilizofanya padri wa awali, Ambrose Mkenda apigwe risasi siku ya mkesha wa Krismasi, mwaka jana ndizo zilizofanya na huyu auawe.
“Polisi wanaweza kujua zaidi kwa sababu tunadhani wanaendelea na uchunguzi kuhusu kupigwa risasi kwa padri Mkenda, watakuwa na fununu za kinachosababisha viongozi wa dini kushambuliwa,” kilisema chanzo chetu cha habari visiwani Zanzibar.
Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Abdalla Mwinyi (kushoto) akijumuika na wananchi kwenye uwanja wa hospitali ya Mnazi Mmoja kufuatia tukio hilo la kuhuzunisha.
Hata hivyo, kuna wengine walikwenda mbali zaidi na kudai kuwa sababu za kupigwa risasi kwa viongozi hao wa kiroho ni itikadi za kidini ambazo uhasama wake unaongezeka kila kukicha hapa nchini.
“Ipo haja kwa serikali kuangalia hili kwani sisi watu wa dini nyingine hapa mjini (Zanzibar) tunaishi kwa wasiwasi,” alisema muumini mmoja wa Kanisa Katoliki.
Padri Cosmas Aman Shayo wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Joseph (kushoto) akijadiliana kuhusu tukio hilo na baadhi ya waumini kwenye uwanja wa hospitali ya Mnazi Mmoja  Zanzibar juzi.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi, ACP Aziz Mohamed alipopigiwa simu alisema atafutwe msaidizi wake ambaye hakupatikana kwa simu.
(Picha Zote na Martin Kabemba, Zanzibar)



Love to hear what you think!