Saturday, May 18, 2013

Zitto: Tafuta Mbunge wako, Mwambie Asikubali Maamuzi haya ya Serikali - Gesi Sio Viazi, Haiozi

Leo wabunge tumealikwa kwenye semina kuhusu sera ya Gesi Asilia. Tumegawiwa tayari nakala zetu, tena zipo kwenye lugha ya kimombo. Ikumbukwe kwamba kuanzia tarehe 22 - 23 Mei 2013 kutakuwa na mjadala wa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini. Semina hii ni maandalizi ya Bajeti hii.

Jambo la kushangaza ni kwamba wakati sera ya Gesi Asilia ipo kwenye rasimu na ndio kwanza wabunge tumeletewa kutoa maoni, Serikali tayari imetangaza tena kugawa vitalu vya Mafuta na Gesi kwenye Bahari kuu na Ziwa Tanganyika Kaskazini.

Zabuni hii mpya ya vitalu vya utafutaji imetolewa wakati kuna maamuzi ya Bunge kuzuia ugawaji huu mpya mpaka sera ya Gesi Asilia na Sheria ya Gesi vikamilike. Haraka hii ya serikali kugawa vitalu bila sera wala Sheria inatoka wapi? Nitashangaa sana wabunge kukimbilia posho za semina hii na kuhalalisha maamuzi yasiyo zingatia maslahi ya Taifa Kwa vizazi vya sasa na vijavyo. Uamuzi wa kugawa vitalu vipya bila kwanza kuwepo Kwa sera na Sheria mpya unapaswa kupingwa Kwa Nguvu zote.

Tafuta mbunge wako, mwambie asikubali maamuzi haya ya serikali.
Tumalize kwanza sera na Sheria ndio tugawe vitalu vipya. Gesi sio viazi, haiozi.



Love to hear what you think!