Thursday, March 28, 2013

MENEJA WA KAMPUNI YA NDEGE YA FASTJET ATIWA MBARONI


MENEJA wa Wafanyakazi wa Ndani ya Ndege wa Kampuni ya Fastjet Emma Donovan, alifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala Dar es Salaam kujibu shtaka linalomkabili la kutoa lugha ya matusi.
Emma (40) alipandishwa kizimbani jana na kusomewa shtaka hilo na Wakili wa Serikali Nassoro Katuga, mbele ya Hakimu Joyce Minde.

Katuga alidai Machi 19 mwaka huu Emma alimtolea lugha ya matusi Samson Itinde jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Emma alikana shtaka hilo ambapo Katuga alidai upelelezi umekamilika na kuomba kupangiwa tarehe kwa usikilizwaji wa awali.
Hakimu Joyce alisema kuwa dhamana ya mshtakiwa iko wazi lakini kwa kuzingatia vigezo vya dhamana vitakavyotolewa kwa kuwa mshtakiwa ni raia wa kigeni.
Alitaja masharti ya dhamana kuwa mshtakiwa anatakiwa kuwasilisha hati yake ya kusafiria au kutoa fedha taslim sh milioni tano na pia awe na wadhamini wawili ambao ni Watanzania.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Aprili 9 ili kupangwa tarehe ya kuanza kwa usikilizwaji wa awali.



Love to hear what you think!