Tuesday, July 31, 2012

Tucta kupinga sharia ya pensheni kwa maandamano


Katibu Mkuu wa Tucta, Nicholus Mgaya
Zaina Malongo
SHIRIKISHO la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta) limeandaa maandamano ya amani kupinga mabadiliko ya  kupitishwa kwa sheria ya marekebisho ya mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA). Maandamano hayo yatafanyika Agosti 4 kuanzia viwanja vya Mnazi mmoja hadi katika Ofisi za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) iliyoko Mikocheni jijini Dar es Salaam.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Tucta, Nicholus Mgaya alisema sheria ya mpya ya mifuko ya jamii inaeleza kuwa mfanyakazi mwanachama atakapotokea kuwa ameacha au ameachishwa kazi hawezi kuchukua mafao yake hadi atakapofikisha umri wa kustaafu ambao ni miaka 55 kwa hiari au miaka 60. Alisema kuwa mfanyakazi mwanachama wa mfuko wowote wa hifadhi ya jamii, akiacha au akiachishwa kazi akiwa na miaka 35 inabidi asubiri kwa miaka 20 alipwe mafao yake ya uzeeni. “Hiki ndio kipelngele cha sheria ambacho kimeleta taharuki kubwa miongoni mwa wafanyakazi wanachma wa mfuko hiyo,” alisema Mgaya.

Alisema wanatambua ukweli kuwa malipo ya uzeeni kwa mujibu wa dhana ya mifuko ya hifadhi ya jamii ni kwa ajili ya kumsaidia mwanachama aliyefikia umri wa uzeeni, hata hivyo walishabaini kuwa dhana hiyo ni vigumu kutekelezeka katika nchi yenye uchumi duni kama Tanzania.
Alisema sababu zinazosababisha ugumu huo ni kutokuwa na uhakika wa ajira, ajira kubwa hapa nchini kuwa mikononi mwa sekta binafsi, na pia mfumo wa hifadhi ya jamii kutokuwa na fao la watu wasiokuwa na ajira.

 Mgaya alisema kutokana na viwazo hivyo, hakuna utaratibu wa hifadhi kwa mwanachama aliyekosa ajira au anayetafuta katika kipindi ambacho ameachishwa kazi na kuhoji kwamba ataishije hadi kufikia miaka 55 kabla ya kupata ajira mahali pengine.

Alisema maisha ya watu hivi sasa yamezungukwa na mazingira hatarishi yenye magonjwa yasiyotibika, ajali nyingi, majanga ya moto mafuriko mambo ambayo yanachangia kwa kiasi kikubwa kupungua kwa umri wa kuishi.

Hata hivyo alisema wanataka kuona mabadiliko ya haraka yafanyike kwenye sheria hiyo ya hifadhi ya jamii ili fao la kujitoa liweze kurejeshwa au uandaliwe utaratibu muafaka utakaohakikisha mwanachama anarejeshewa michango yake na ya mwajiri pamoja na riba mara tu anapokoma uanachama wa mifuko hiyo.

Alisema Tucta haitasita kuchukua hatua za kisheria endapo mamlaka itaendelea kushikilia msimamo wake wa kubakiza kifungu hicho kinachomtaka mwanachama wa mfuko afikishe miaka 55 ndio alipwe mafao yake.

Aidha alisema Tucta wamesikitishwa na kushangazwa na kuwahi kutangazwa kwa mabadiliko ya sheria hiyo ya hifadhi ya jamii huku mchakato wake ukiwa bado haujakamilika baada ya kuridhiwa na Rais kama kupitia kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na kutangaza kwenye gazeti la Serikali.

Mgaya alisema Tucta inataka mamlaka ya mdhibiti na msimamizi wa mfuko wa hifadhi ya jamii kuchukua jukumu la kutoa elimu kwa wanachama kuhusu sheria hiyo mpya kusaidia kupunguza malalamiko yasiyo ya lazima.

 Kwa upande wa Tucta Mkoa wa Dar es Salaam, Mratibu Musa Mwakalinga alisema wanapinga mabadiliko hayo kwani mishahara ya wafanyakazi walio wengi haiwatoshelezi hivyo watakosa mtaji wa kuanzisha ujasiriamali au kujiajiri wenyewe na kujikwamua baada ya ajira kukoma. Alisema mabadiliko hayo yataongeza umasikini kwa wafanyakazi pindi watakapoachishwa au kuacha kazi, wafanyakzi wengine watakaotaka wajiajiri wenyewe pindi ajira yao itakapositishwa.
 Alisema sheria hiyo inakusudia kutotoa huduma bora zitakazokidhi mahitaji mbalimbali ya msingi wa wafanyakazi ambao ni wanachama wa mifuko hiyo inayojali zaidi wafanyabiashara, ambao sio wenye mifuko kwa kuwajengea vitega uchumi ambavyo havimnufaishi mwanachama moja kwa moja.   MWISHO


Love to hear what you think!