Waandishi Wetu
MCHAKATO wa uandikishaji wa Vitambulisho vya Taifa
jijini Dar es Salaam umeingia dosari, baada ya baadhi ya waandikishaji
na maofisa wa serikali za mitaa kuwatoza wananchi fedha kinyume cha
sheria.Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi katika maeneo kadhaa ya Jiji
la Dar es Salaam umebaini kuwa, mfumo wa utambuzi umekuwa ukitumiwa na
baadhi ya maofisa na viongozi wa serikali za mitaa kuwatoza wananchi
fedha.
Hali hiyo imewakatisha tamaa baadhi ya watu na kuwafanya
wahoji kama kuna kitu watakosa wasipokuwa na kitambulisho hicho.Mpango
huo mbaya ya kuwatoza fedha wananchi unafanywa wakati ambapo Mamlaka ya
Vitambulisho vya Taifa (Nida) inasisitiza kuwa uandikishaji huo ni bure
na kuwa mwananchi yeyote hapaswi kutozwa fedha au gharama nyingine
zozote.
Wananchi kadhaa waliozungumza na gazeti hili kwa nyakati
tofauti jana na juzi, jijini Dar es Salaam, walithibitisha kwamba
walitozwa kati ya Sh500 na 3,000. Baadhi ya wakazi wa maeneo ya Temeke,
Ilala na Kinondoni walilalamika kuwa, maofisa waandikishaji wanawatoza
kati ya Sh500 na 1,000 ili waandikishwe.
Uchunguzi huo umebaini
pia kuwa, maofisa wa ofisi za kata na mitaa wanatoza fedha kati ya
Sh1,000 na 3,000 kwa watu ambao hawana vitambulisho, kama vile kadi ya
mpigakura, cheti cha kuzaliwa, ubatizo au hati ya kusafiria.
Baadhi
ya maofisa waandikishaji wanadaiwa kuwa, wanawaelekeza baadhi ya watu
kwenda kupata barua ya za utambulisho katika ofisi za serikali za mtaa,
au mtendaji ili kuthibitisha kuwa wao ni raia.
Baadhi ya wananchi wanadai walilipa fedha walizodaiwa kwa vile zoezi hilo ni mpango uliowekwa na Serikali.
Hata
hivyo, imebainika kuwa wale ambao hawana uwezo waliacha kujiandikisha
kwa imani kuwa hakuna watakalopoteza au kupata wakiwa na vitambulisho
hivyo vya taifa, au wasipokuwa navyo.
Ashura Ally (32) mkazi wa
Tabata Kisiwani wilayani Ilala, ambaye ni mmoja wa waliotakiwa kutoa
fedha na ofisi ya serikali za mtaa alisema: “Mimi sina kitambulisho wala
kitu chochote, lakini tatizo ni kuambiwa nikienda serikali za mitaa
kuandikiwa niwe na Sh3000. Siwezi kutoa.”
Mkazi mwingine wa
Tabata, Neema Shao (28) alilalamika kutumia muda mwingi kwenye foleni
akisubiri kujaza fomu ya uandikishwaji. “Mtu mmoja anatumia dakika zaidi
ya kumi kuandikishwa. Baadhi ya watu wameondoka kwa sababu ya kusubiri
muda mrefu,” alisema Neema.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Wailes, Abdon
Kidege alisema changamoto kubwa anayoiona ni watu kupuuzia zoezi la
uandikishaji. “Baadaye tuliamua kuanza kutoa elimu kuhusu umuhimu wa
kazi hii. Walidhani ni jambo la kawaida tu lakini baada ya hapo walianza
kujitokeza,” alisema.
Wakati huohuo, Mzee Rajabu Hakungwa (72)
mkazi wa Mtaa wa Kilimahewa iliyopo Tandika alisema kuwa, wakazi wa
eneo hilo hawakuwa na elimu juu ya umuhimu wa kuandikisha.
“Awali,
wakazi wa mtaa wetu hawakutambua umuhimu wa zoezi hili, lakini baada
ya kuelimishwa kwa sasa wanaongezeka,” alisema Mzee Hakungwa.
Mkazi wa Tabata Kimanga, Prasido Kombe alisema huenda muda uliowekwa na Nida usitoshe kutokana na uandikishaji kwenda polepole.
“Tunaiomba
Nida iongeze muda kwani tunasikia siku ya mwisho kujiandikisha ni
Jumapili. Kama itakuwa hivyo na kasi ya watendaji ni ndogo watu wengi
watakosa nafasi ya kujiandikisha,” alilalamika Kombe.Mkazi mwingine wa
Tabata Kisiwani, Abduly Juma alisema bado wananchi hawana elimu ya suala
hiyo ndiyo maana wengi wao wamekuwa wakipuuzia kwenda kujiandikisha.
Kauli ya NIDA
Msemaji
wa Nida, Rose Mdami alisema kuwa mwananchi yeyote hapaswi kutoa fedha
yoyote ili kufanikisha mkakati wa kuandikishwa, hivyo akawaonya maofisa
waandikishaji na wale wa serikali za mitaa kuacha tabia hiyo.
Alisema Nida imekuwa ikifuatilia kwa karibu utendaji huo na kukiri kuwa dosari hizo zipo na baadhi maofisa wamewatia mbaroni.
“Tumefanikiwa
kumkata mmoja wao katika Kituo cha Yombo Buza kilichopo Mtaa wa Sigara,
Kata ya Tandika wilayani Temeke,” alisema Mdami. Imeandikwa na Aidan
Mhando, Kelvin Matandiko na Zakhia Abdallah